visit here again on mukebez.blogspot.com


CHANGE YOUR LIFE

CHANGE YOUR LIFE
Go to Amazon .com and get the copy of this book to make your life better.

Alhamisi, 3 Julai 2014

MAKAMBA KUGOMBEA URAIS 2015

Dar es Salaam.Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba ametangaza nia yake ya kuwania urais akisema huu ni wakati wa kupisha fikra mpya kuongoza dola, licha ya chama hicho kuzuia kutangaza nia na kupiga kampeni kabla ya muda.
Makamba, mmoja wa makada wa CCM walioonywa na chama hicho baada ya kutuhumiwa kuanza kampeni mapema, alijipigia debe kuwa iwapo atapitishwa na chama hicho, ataelekeza nguvu kwenye vipaumbele vyake vinne ambavyo ni ajira, huduma za jamii, uchumi imara na utawala bora.
Mbunge huyo wa Bumbuli alisema hayo akiwa Uingereza anakohudhuria mkutano wa sekta ya mawasiliano baada ya kuhojiwa na Shirika la Utangazaji la Uingereza na baadaye kufafanua nia hiyo katika mahojiano na Mwananchi jana.
“Ni wakati wa fikra mpya kushika dola na mimi ninaona kwamba wazee wakae kando. Mfano awamu moja inapoondoka na wazee walioko katika mfumo wakae kando ili kupisha fikra mpya kuongoza dola,” alisema Makamba ambaye ana umri wa miaka 40.
Mwandishi huyo wa zamani wa hotuba za Rais Jakaya Kikwete, alisema hadi sasa ameshafanya uamuzi kwa asilimia 90 kujitokeza kuwania nafasi hiyo ya juu kuliko zote nchini, bado asilimia 10 katika baadhi ya mambo ambayo anaendelea kuyatafakari, kuzungumza na makundi mbalimbali ya wazee, viongozi wa dini na viongozi waliopita “ili nipate ushauri wao kuhusu namna ya kufanya jambo hili”.
Alipoulizwa iwapo ameshawishiwa au kushinikizwa na watu au ni utashi wake binafsi, Makamba alisema kuwa yote ni mchanganyiko.
“Huwezi kuamka nyumbani na kusema unakwenda kugombea. Kuna msukumo wa wapambe wachache ambao ni lazima ukapime kwa makini kabla ya kuchukua hatua yeyote,” alisema.
“Nchi nzima unakuta inazungumza uwe rais, lazima upime na chagizo hizo ni za kweli au zinatoka wapi. Lakini unaposikia hadi viongozi wa dini, wanafunzi wa vyuo unapokwenda wanakuuliza jambo hilo hilo, unatakiwa utafakari.”
Aliongeza: “Mfano unakwenda Maswa (Shinyanga), Liwale (Lindi), Simanjiro (Kilimanjaro), Wete (Pemba) unaambiwa unafaa, ni muhimu katika hili lakini pia wazee, vijana, viongozi wa dini wanasema unafaa kuwaunganisha Watanzania wote ni jambo la kulitafakari na kulichukulia hatua.”
Februari mwaka huu, Kamati Kuu ya CCM iliwapa onyo kali makada wake sita akiwemo January Makamba ikiwatuhumu kupiga kampeni za urais kwa ajili ya uchaguzi mkuu ujao kabla ya muda.
Makada wengine waliopewa adhabu hiyo ni mawaziri wakuu wa zamani, Frederick Sumaye na Edward Lowasa, Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Mahusiano na Uratibu), Stephen Wassira na mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.
Pia makamu mwenyekiti wa CCM, Philip Mangula aliwahi kukemea tabia ya baadhi ya wana-CCM kutangaza mapema nia ya kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika uchaguzi ujao, akisema ni wasaliti wakubwa ndani ya chama.
MWANANCHI

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni