visit here again on mukebez.blogspot.com


CHANGE YOUR LIFE

CHANGE YOUR LIFE
Go to Amazon .com and get the copy of this book to make your life better.

Jumapili, 24 Agosti 2014

BWANA MAJENGO PENDA UNATAKA UKUU WA NCHI LAKINI???....

Du! Kweli hii balaaa,nimeona tena kwenye vyombo vya habari kuwa bwana MAJENGO PENDA kuwa na wewe umetangaza nia ya kutaka kuwa mkuu wa nchi hii!!.

Hahahaa hongera sana nafikiri inawezekana wewe kuwa mkuu wa nchi kwasababu una sifa ya kutokuwa na kashfa,huna makundi na una busara kiasi fulani ingawa umeshindwa kuukwepa mtego wa siasa za uchama.

Swali langu kwako mzee wangu ni kuwa je umejipanga kweli kupambana na kundi kubwa la watu zaidi ya kumi ambao nao wanawania nafasi hiyo akiwepo mheshimiwa mstaafu ambae sasa makanisa na misikiti vinafahamu pesa zake vya kutosha na anaonekana ameshaingia mpaka kwa wasanii kupata sapport??

Unaonekana kuwa na busara je utaweza siasa za kumwaga pesa kwa wananchi ili baadae ukipata uchukue chako mapema??

Waswahili wanasema ukiona panafuka ujue panaungua,na ukiona mtu anatangaza nia hadharani ujue tayari ameshajipanga kikamilifu,na ndio mana mimi nataka kugombea kama mgombea binafsi lakini sijatangaza nia bado kwasababu bado nakusanya signature! Lakini mzee wangu unahisi unaushawishi wa kutosha kweli kumzidi mheshimiwa ALIYELOWA SASA?.

Mhh mimi sijui bana labda ukiona au yoyote ayakaesoma hapa akikuambia kuhusu maswali yangu unaweza kuamua kunijibu kijana wako mana napata shida sana na huyo jamaa,hao wengine sina shida nao unaweza kuwapiga chini.

Hongera sana najua tutakutana kwenye kampeni mimi nikiwa mgombea binafsi na wewe ukigombea kwa tiketi ya CHUKUA CHAKO MAPEMA.SORRY.

Ijumaa, 22 Agosti 2014

CLOUDS FM YAPIGWA FAINI KWA KUWADHALILISHA MABIBI

Mamlaka ya Mawasiliano Tanzania (TCRA), imetoa onyo pamoja na kutoza faini ya takribani Sh milioni 5 kwa kituo cha redio na televisheni cha Clouds, kwa kukiuka kanuni za utangazaji za mwaka 2005.
Wakielezea uamuzi huo jana jijini Dar es Salaam, Kamati ya Maudhui ya mamlaka hiyo ikiongozwa na Mwenyekiti wake, Margaret Munyagi ilisema kuwa ukiukwaji wa kanuni hizo ulifanywa kwa nyakati tofauti na vituo hivyo.
Alisema kwa upande wa kituo cha redio cha Clouds, kupitia kipindi chake cha ‘Njia Panda’ kilichorushwa hewani Juni 15 mwaka huu kati ya saa 8.00 mchana na saa 10.00 jioni kilikuwa na mada iliyohusu safari ya kuzimu ambapo maudhui yake yalijaa simulizi za kufikirika, za kishirikina na kichawi.
Aidha alisema kosa lingine kituo hicho hakikufuata kanuni za Utangazaji(maudhui) za mwaka 2005 zinazowataka kuwasilisha ratiba ya vipindi vyao kwa TCRA ili viidhinishwe na vilevile kuvichapisha katika gazeti kabla ya kurushwa hewani ambapo kipindi cha Njia Panda hakikuwasilishwa kwa ajili ya kuidhinishwa.
Wakati huo huo, kituo cha televisheni cha Clouds kilirusha kipindi cha ‘Bibi Bomba’ Mei 16 na Juni 6 mwaka huu kati ya saa 3.00 na saa 4.00 usiku ambacho kilikiuka kanuni za Utangazaji (maudhui) za mwaka 2005.
Alisema kipindi hicho kilidhalilisha mabibi hao walioshiriki pamoja na wanawake kwa ujumla kutokana na maswali ya aibu waliyokuwa wakiulizwa na waamuzi wa shindano hilo ambayo ni kinyume na kanuni hizo.
Aidha alisema kituo hicho kinatozwa faini ya Sh milioni moja na kutakiwa kuwasilisha TCRA mwongozo wa kuchuja na kusimamia maudhui yasiyofaa kabla ya kutangazwa.
TCRA imesema kama Kanuni za Utangazaji zitaendelea kukiukwa hatua kali zaidi za kisheria zitachukuliwa dhidi yao.

BILA MILION 20 DIAMOND HAFANYI SHOW

Tangu mwaka juzi tulifahamu kuwa Diamond Platinumz ndiye msanii wa Tanzania anaelipwa kiasi kikubwa cha pesa, na mwaka jana ikaelezwa kuwa bila milioni 10 au 8 za Kitanzania humpati kwenye show yako.
Lakini kiwango kipya kilichotajwa jana kitawapa kizunguzungu zaidi hasa mapromota wenye mitaji midogo wenye ndoto za kufanya kazi na mwimbaji huyo.
Kwa mujibu wa, Babu Tale ambaye ni meneja wake, hivi sasa kiwango cha chini anachochaji kwa show moja hapa nchini ni $15,000 (sawa na shilingi Milioni 25 za Tanzania).
“Tuna show Marekani show kumi na tano (15), show kumi na tano dola elfu ngapi? Na kwa hapa Tanzania hatufanyi show chini ya dola e15,000.”Babu Tale aliiambia Bongo5.
Kwa mujibu wa Babu Tale, wanachaji kiasi cha hadi dola 25,000 kwa show moja za nje ya nchi (ikiwemo Marekani).
“Tunalipwa milioni 20 show moja, tunalipwa dola elfu 25,000 show moja, hii ni zaidi ya madawa ya kulevya.”Alisema wakati akikanusha tuhuma kuwa Diamond anauza dawa za kulevya.
Kwa mahesabu ya haraka haraka, shows 15 mara dola 25,000 ni sawa na $375,000 (Sawa na shilingi za Tanzania 625,687,500).
Yesss! Ni zaidi ya Milioni mia sita ishirini na tano za kitanzania. Kama ni kweli, basi Diamond anastahili kweli kuitwa Dangote wa Bongo Flava.
Bado michongo inaendelea kumiminika ambapo hivi karibuni meneja wa Trey Songz alimtumia ujumbe kuwa atakapokuwa na nafasi amshitue waongee.

MBUNGE WA CCM AJIUNGA UKAWA

Dodoma.Jana ilikuwa kama sinema pale viongozi wa Kamati Namba Moja ya Bunge Maalumu walipojikuta wakibishana na mjumbe wao mbele ya waandishi wa habari, huku siri za mambo ya ndani ya vikao zikianikwa hadharani.
Kamati hiyo inaongozwa na Naibu Waziri, Ofisi ya Makamu wa Rais, Ummy Mwalimu na makamu wake ni Waziri wa Sayansi na Teknolojia, Profesa Makame Mbarawa, huku ikiwa imesheheni vigogo wengine wakiongozwa na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda.
Viongozi wengine katika kamati hiyo ni Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu (Uhusiano na Uratibu), William Lukuvi, Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Utawala Bora), George Mkuchika na Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Dk Hussein Mwinyi.
Wamo pia Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii, Dk Seif Rashid, Waziri wa Kazi na Ajira, Gaudensia Kabaka na Naibu Waziri wa Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto, Dk Pindi Chana.
Jana asubuhi, Mwalimu na Profesa Mbarawa walifika mbele ya waandishi wa habari katika Hoteli ya St Gasper wakiwa wameambatana na mmoja wa wajumbe wa kamati hiyo ambaye pia ni Mbunge wa Nkasi Kaskazini (CCM), Ally Keissy.
Lengo la mwenyekiti na makamu wake lilikuwa ni kumbana Keissy ili akanushe taarifa aliyoitoa juzi kwenye moja ya televisheni kwamba kamati hiyo inaongoza kwa kuvunja kanuni hasa katika suala la akidi ya vikao kutotimia.
Sinema ilivyoanza
Walipofika mbele ya waandishi wa habari, Keissy alipewa fursa ili akanushe taarifa yake, lakini alibadili mada na kuanza kuzungumzia masuala ya muundo wa Serikali na Bunge, huku akisema yeye ni muumini wa serikali tatu na siyo mambo ya serikali mbili zinazopendekezwa na wengi kutoka katika chama chake.
Kauli hiyo iliwashtua Mwalimu na Profesa Mbarawa ambao walianza kumkatisha ili asiendelee.
“Keissy sikukuitia mambo hayo, huu ni mkutano wangu, naomba ukanushe nilichokuitia, hayo utazungumza baadaye tafadhali sana,” alisema Mwalimu.
Wakati huo Profesa Mbarawa na waandishi wa habari waliokuwapo walivunjika mbavu kwa vicheko, huku yeye akiendelea kusisitiza kwamba ni muumini wa Tanganyika.
Wakati akisema hayo, Profesa Mbarawa naye aliingilia kati na kumtaka Keissy kueleza kilichompeleka hapo huku akimtaka aache kelele za kupotosha wananchi kwa kuwa anachosema siyo kweli.

WIZARA YAFUTA AJIRA ZA UHAMIAJI

Dar es Salaam. Wizara ya Mambo ya Ndani imefuta ajira 200 za konstebo na koplo katika Idara ya Uhamiaji baada ya kubaini kuwa kulikuwa na upendeleo katika usaili na sasa zitatangazwa upya na kusimamiwa na wizara hiyo.
Akizungumza Dar es Salaam jana, Katibu Mkuu wa wizara hiyo, Mbarak Abdulwakil alisema hatua hiyo imechukuliwa baada ya kamati maalumu ya kuchunguza ajira hizo kubaini wazi kwamba waliopewa nafasi hizo hawakukidhi vigezo.
Abdulwakil alisema wizara imesikitishwa na udhaifu huo baada ya kubainika wazi kwamba malalamiko yaliyotolewa na wananchi na kusababisha wizara kuingilia kati na kufuta usaili wa kuitwa kwenye ajira kwa watu 200 ulikuwa sahihi.
Alisema baada ya kubainika kwamba kweli kulikuwa na upendeleo wa dhahiri kwani watahiniwa wenye sifa na waliopata alama za juu wakati wa usaili hawakuitwa na kukiukwa kwa vigezo vya wazi, ajira hizo zitatangazwa upya na kusimamiwa moja kwa moja na wizara na siyo idara hiyo kama ilivyokuwa awali.
“Kamati hiyo iliyoanza kazi yake Agosti Mosi, mwaka huu ilibaini kwamba hata kigezo cha umri, ambacho ni miaka 25 kwa konstebo na miaka 30 kwa koplo hakikuzingatiwa kwani wenye umri zaidi ya huo waliitwa kazini... “Lakini zaidi, baadhi ya wasailiwa walioitwa kazini ni ndugu na jamaa wa watumishi wa Idara ya Uhamiaji,” alisema.
Alieleza kwamba utaratibu mpya wa kuwapata watu wanaostahili utatangazwa kupitia vyombo vya habari na mamlaka ya usimamizi imerejeshwa kwenye wizara husika badala ya kuachiwa kwenye idara husika.
Alisema pamoja na kwamba miongoni mwa udhaifu uliobainika ni kwamba matangazo ya kazi yaliyotolewa kwenye vyombo vya habari hayakuainisha viwango na madaraja ya ufaulu kwa waliomaliza kidato cha nne na cha sita, lakini hata wale waliofanya vizuri katika usaili hawakuitwa kazini na hakuna sababu maalumu zilizotolewa.
Alisema ajira hizo zilizofutwa zinahusisha pia nafasi 28 zilizokuwa zimetangazwa kupitia Idara ya Uhamiaji Zanzibar.
Alisema si kosa kwa ndugu na jamaa wa watumishi wa Idara ya Uhamiaji kuajiriwa katika nafasi hizo iwapo wanakidhi vigezo vyote, lakini inapotokea kwamba hakuna msimamizi huru ni wazi kwamba kunakuwa na upendeleo kama ilivyotokea na idara hiyo haichukui watumishi kutoka Sekretarieti ya Ajira, kwa kuwa wanaohitajika ni askari.
Ajira hizo zilitangazwa Februari 17, mwaka huu na watu 15,707 walijitokeza kuwania nafasi hizo 200, miongoni mwao, waombaji 1,005 waliitwa kwenye usaili na 200 waliothibitishwa waliitwa kazini.
Hata hivyo, baada ya tangazo la kuitwa kazini malalamiko yaliibuka kupitia vyombo vya habari na baadhi ya mitandao ya kijamii, kwamba baadhi ya walioitwa katika ajira hizo walikuwa ni watoto, jamaa na ndugu wa maofisa wa Idara ya Uhamiaji.
Baada ya kuibuka kwa malalamiko hayo, wizara iliingilia kati na kuunda kamati hiyo ya watu watano Julai 31, ambayo ilipewa siku 10 kukamilisha kazi yake na kutoa matokeo.

CHADEMA WATUNGA WIMBO MAALUM KWAJILI YA MAANDAMANO YA UKAWA

CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimetunga wimbo maalumu kwa ajili ya maandamano yaliyopangwa na chama hicho na vyama vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA) ili kushinikiza Bunge Maalumu la Katiba ambalo linaendelea Mjini Dodoma, lisitishe vikao vyake hadi kuwepo maridhiano.
Wimbo huo ambao ni mahususi kwa ajili ya maandamano ambayo haifahamiki yatafanyika lini, umepangwa kusambazwa kwa wananchi nchi nzima ukifahamika kama mchakamchaka wa katiba.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mkurugenzi wa Mawasiliano wa chama hicho, Bw. John Mnyika, alisema wimbo huo utaimbwa na wananchi pamoja na wanachama wa vyama vinavyounda UKAWA na kuuimba mbele ya waandishi wa habari.
"Msimamo wa kuandamana nchi nzima uko palepale, tarehe rasmi ya maandamano itatangazwa baadaye...kutungwa kwa wimbo huu ni maandalizi ya awali tukisubiri matokeo ya mazungumzo ambayo yanaendelea nyuma ya pazia.
"Kama hakutakuwa na maridhiano katika mazungumzo hayo, tutaingia rasmi barabarani ili kufanya maandamano...lengo letu ni kutaka maridhiano au mchakato huu usitishwe,"alisema.
Aliongeza kuwa, Kamati Kuu ya CCM kupitia Mwenyekiti wa chama hicho Taifa, Rais Jakaya Kikwete, amekosea kutoa uamuzi wa kubariki mchakato huo uendelee badala ya kuusitisha.
Alisema CCM kimedhihirisha msemo wa Baba wa Taifa, Hayati Mwalimu Julius Nyerere kuwa;"Bila CCM thabiti nchi inalegalega", hivyo nchi imeanza kulegalega kutokana na udhaifu wao.
"Kimsingi mchakato huu unapaswa kusimama ili kupisha maridhiano kwanza, kuendelea kwake ni matumizi mabaya ya fedha za Watanzania...sisi tunataka Bunge lisitishwe,"alisema.
Bw. Mnyika alisema ni vyema Rais Kikwete ajitokeze hadharani kuzungumza na wananchi kama alivyo ahidi awali kuwa kama majadiliano yaliyokuwa yakiendelea yakikwama, angeingilia kati ili suluhu iweze kupatikana.
Aliongeza kuwa, CCM kimefuata masilahi yao katika mchakato huo na kuyapuuza mapendekezo ya wananchi hivyo kusababisha nchi ilegelege kutokana na uongozi uliolegalega.
Aliitaka Serikali ya chama tawala, kulinusuru Taifa katika mchakato huo kwa kutafuta maridhiano au kulisitisha Bunge hilo.

Jumapili, 17 Agosti 2014

BWANA LESSO HILI LA URAIS UMECHEMSHA

Hahahaaa!Habariyako bwana Lesso.Niliona hivi karibuni umefunguka kwenye vyombo vingi vya habari kwamba chama chako cha Domo kikikuruhusu unataka kuwa kiongozi wetu wa nchi!!.
Hahahaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaaa!usitake kunivunja mbavu!wewe ukakae Ikulu.Patakalika kweli??.
Najua katiba inasema kila mtanzania ana haki ya kuwa kiongozi,lakinipia usisahau kuwa kila mtanzania au binadamu ana kipaji chake na kwamba kuna eneo akikaa anafanya kwa ufanisi mkubwa.
Kwa maoni yangu wewe ufanisi wako uko mjengoni na huwa unachangamsha sana na kuleta changamoto uwapo pale mjengoni kwahiyo endelea kuwa pale kwasababu huku unakopataka hapakufai mjengo utapooza.
Hebu pata picha bila wewe nani atapiga kelele kule?au walinzi wa pale mjengoni watafanya kazi gani katika harakati za kutoa watu mjengoni.
Usifanye makosa aliyofanya mwenzako SULAA alipoamua kuacha mjengo na kutimkia urais wakati by then mjengo ullipamba moto.
Kumbuka mzee huyu alikuwa ukimuona na mkoba tu mjengoni ujue ana nyaraka anakuja kuripua jipu na mambo kweli yalikuwa yananyooka lakini mala baada ya kukosa u presidaaa mjengoni hayupo na wala hasikiki zaidi ya mitaani mpaka tunatamani arudi mjengoni.
Kwa hilli bwana Leso niseme kuwa umechemsha na upresidaa sio fani yako wewe endelea kufanya drama Bungeni na kuendelea kulichangamsha mambo yakae sawa.
Ni kwa nia ya kuwekana sawa kwahiyo usijenge chuki yoyote kwa kuwa mimi si mnazi wa chama chochote na haijulikani nani anafuata katika safu hii.tchao.

Alhamisi, 14 Agosti 2014

UFAHAMU UGONJWA WA EBOLA NA DALILI ZAKE

Ebola ni ugonjwa wa hatari unaosababishwa na virusi vijulikanavyo
kwa lugha ya kitaalamu “Ebola Virus”. ugonjwa wa damu kutoganda.
Ugonjwa huu ni miongoni mwa magonjwa yajulikanayo kwa ujumla kama Homa za Virusi zinaazosababisha kutokwa na Damu mwilini,(Viral Haemorrhagic Fevers) Chanzo kamili cha virusi vya ugonjwa
huu hakijulikani. Katika orodha ya watu 10 waliopata kirusi cha Ebola, basi wastani kati ya watano au tisa hufa.
Hali inayosababisha mlipuko wake pia haijulikani.Ugonjwa huu pia hauna tiba wala chanjo.Hata dawa za jadi hazijathibitika kutibu ugonjwa huu.
Dalili za Ebola
Pale watu wanapopata Ebola, dalili zake za kwanza ni kuonekana kama magonjwa mengine
Dalili za ugonjwa huu ni:-
Homa kali, inayoambatana na kutokwa damu katika matundu yote ya mwili kama pua, njia ya haja kubwa na dogo, mdomoni, masikioni, machoni n.k.
· Kutapika damu
· Kuharisha damu
· Fizi kuvuja damu
· Kutokwa na damu na kuvujia chini ya ngozi. Kwasababu ya kutokwa na damu sehemu za haja kubwa na ndogo, choo na mkojo pia vitaonekanakuwa na damu.
Kuenea kwa Ebola.
Ugonjwa huu unaenea kwa urahisi sana na haraka kutoka mtu mmoja hadi mtu mwingine kupita njia mbali mbali.
Njia hizi ni:-
· Kuingia mwilini au kugusana na:-
· Mate
· Damu
· Mkojo
· Machozi
· Kamasi
majimaji mengine ya mwili, ikiwa ni pamoja na jasho. kugusa mtu aliyekufa kwa ugojnwa wa Ebola kushika/kugusana na wanyama jamii ya nyani. · Kuchomwa na sindano au vifaa ambavyo havikutakaswa Ugonjwa huu pia huambukizwa kwa njia ya
kujamiiana. kugusa taka ngumu au maji taka yaliyotokana
na kumhudumia mgonjwa Ebola.
Athari za ebola
· Unasambaa kwa haraka sana Unasababisha vifo vingi kwa muda mfupi · Jamii huingiwa na hofu na wasi wasi na kushindwa kufanya shughuli zao za kawaida ni gharama kuwahudumia/kutibu wagonjwa. · Mipaka inaweza kufungwa na watu wakashindwa kusafiri kutoka eneo/nchi moja hadi nyingine.
Tiba ya Ebola
Hakuna tiba maalumu ya homa ya Ebola. Lakini ikiwa watu wanapata huduma bora kutoka kwa madaktari na wauguzi, wengi wao huishi.
Kinga ya Ebola
Ugonjwa wa Ebola unaweza kuzuilika.Ni muhimu kwa kila mmoja kuwajibika Njia kuu za kujikinga na ugonjwa huu:-
Kuepuka kugusa au kuingiwa na mate, damu, mkojo, jasho, kinyesi, machozi na maji maji mengine yanayotoka mwilini mwa
mwenye dalili za ugonjwa wa Ebola. Kwa kuwa ugonjwa huu pia huambukizwa kwa njia ya kujamiiana, epuka kuwa na
mpenzi zaidi ya mmoja.
Kutoa taarifa mapema kwa viongozi wa serikali na wa huduma za Afya katika ngazi zote pale anapotokea mtu mwenye dalili za
Ebola
uwahi katika vituo vya huduma za Afya pale mtu anapoona dalili za ugonjwa huu. Wananchi wana tahadharishwa kuepuka
kushughulikia maiti ya mtu aliyekufa kwa Ebola;badala yake watoe taarifa kwa uongozi wa kituo cha huduma za Afya kwa ushauri.
ufanya ufatiliaji madhubuti wa ugonjwa huu. Wananchi waepuke mila na desturi zinazoweza kuchelewesha kupata huduma
muhimu na kuzidi kueneza ugonjwa wa Ebola
Wagonjwa wa Ebola hutengenishwa na wagonjwa wengine ili
wasipate kuambukizwa.
Zingatia usafi wa mwili na tabia.
KUMBUKA
Ugonjwa wa Ebola ni hatari sana. Unasambaa haraka na unasababisha Madhara na vifo vingi. Epukana nao.

TAARIFA YA UGONJWA WA EBOLA KUTINGA TANZANIA

Mhudumu wa afya akiwa katika hali ya tahadhari ya Ebola huko Afrika Magharibi
Kuna taarifa ya kuwepo kwa mtu mmoja anayehisiwa kuwa na virusi vya ugonjwa wa Ebola nchini Tanzania.
Kwa mujibu wa Mkuu wa Kitengo cha mawasiliano wa Wizara ya Afya ya Tanzania Nsachris Mwamaja mtu huyo ana asili ya Afrika Magharibi ambaye ni mkazi wa mji wa Dar es Salaam ambaye alifika katika hosptali moja akiwa na homa kali ikiwa ni dalili mojawapo ya ugojwa huo .
Bwana Mwamaja amesema mgonjwa huyo ambaye ni mtoto wa makamo tayari ameshatengwa na yupo chini ya uangalizi wa karibu madaktari katika hosptali Temeke ambayo ni ndio iliyotengwa kwa ajili ya watakaohisiwa kuwa na ugonjwa huo.
Amesema sababu nyingine ya kuhisiwa kwa mtu huyo kuwa huenda ameambukizwa virusi vya ugonjwa huo ni kwa vile hivi karibuni alitokea nchini Benin.
Hii ni mara ya kwanza ya kuwepo kwa taarifa za mtu kuhisiwa kuwa na virusi vya Ebola nchini Tanzania.
Taarifa hizi zinakuja baada ya hapo awali serikali ya nchi hiyo kukanusha taarifa iliyotolewa na gazeti moja la udaku kuwa kuna mgonjwa mmoja wa Ebola aliyegundulika nchini Tanzania.

Jumatano, 13 Agosti 2014

UMAKINI UNAHITAJI KUONGEZWA SERIKALINI

SERIKALI IJIPANGE KUZUIA MATUKIO YANAYOHATARISHA AMANI
Na Deonidas Mukebezi(UDSM)
Inakuwa haiingii akilini pale ambapo Serikali imekuwa ikihubiri kuwa Tanzania ni nchi ya amani ndani nan je ya nchi wakati kuna matukio yanayoashiria waziwazi kuwa amani inayohubiliwa kila siku na Serikali katika vyombo mbalimbali vya habari haipo kama inavyosemwa.
Katika nchi hii tumekuwa tukishuhudia mfululizo wa matukio mbalimbali ya kusikitisha na ambayo si ya kiubinadamu kama yale ya kuwaua vikongwe kwa tuhuma kuwa ni wachawi,mauaji ya walemavu wa ngozi ambao viungo vyao vimekuwa vikitumiwa kwa imani za kishirikina pamoja na mauwaji au uteswaji wa waandishi wa habari,matukio ambayo yamekuwa yakiibuka na kuondoka kama mitindo ya fasheni za nguo .
Pamoja na matukio yote hayo katikati ya mwezi wasaba mwaka huu yameibuka matukio mengine ya wizi wa watoto ambao haijulikani wahusika wanawaiba kwa minajiri gani ingawa wizi huo umekuwa ukienda sambamba na vitendo vya watoto kufanyiwa vitendo vya kikatili.
Mfano wa watoto ambao wameshapotea mpaka sasa ni pamoja na mtoto Merryn Reppyson ambae aliibwa na mtu asiefahamika eneo la Changanyikeni karibu nachuo kikuu cha Dar es salaam jijini Dar es salaam julai 15 na ambae mpaka sasa hajapatikana.
Jambo la kusikitisha ni kwamba wakati polisi wanasema wanafuatilia tukio moja,tukio jingine la aina hiyohiyo linaibuka.
Jambo hili linaumiza sana hususani wazazi wa watoto,lakini pia jamii ambayo sasa imekuwa ikiishi kwa hofu kuwa pengine watoto wao pia wanaweza kuingia katika kadhia hiyo.
Ni wazi kuwa jamii imechoshwa na matukio haya nan i jukumu la serikali kuwa na mipango endelevu ya kuhakikisha kuwa hayaibuki matukio ya ajabu ajabu ambayo yanaonekana dhahiri shahiri kuitikisa amani ya taifa letu ambayo imekuwa ikihubiliwa kila leo.
Pia serikkali inapaswa kutafuta na kutoa majibu sahihi pale ambapo wananchi walioipa dhamana kukaa madarakani wanapouliza maswali yanayotaka majibu ya haraka badara ya kubweteka na kufanya kazi kwa mazoea kwani wakati hausuburi na ya jana sio ya leo wala ya leo sio ya kesho.

Jumatatu, 11 Agosti 2014

SOMA HII YA MWANAFUNZI ALIYETEKWA NA KUFNYISHWA NGONO

Kweli dunia ina mambo! Kuna watu wanajaribu kutumia kila fursa inayopatikana kujinufaisha kwa kupata fedha hata ziwe 'chafu', kwao kitu cha maana ni kupata utajiri kwanza.
Kundi la watu wanaofanya biashara ya kusafirisha watu, wamekuwa wakitumia fursa ya ukosefu wa ajira kama chambo cha kuwanasa vijana na kuwaingiza kwenye biashara haramu kama ukahaba.
Hivi karibu kundi hilo linalosafirisha watu lilipita katika vyuo vikuu kadhaa nchini Uganda na kuwaahidi wanafunzi kuwa lingewatafutia kazi Ulaya na Marekani, kwani lina uzoefu wa kutosha na kazi hiyo. Mmoja wa vijana 'waliobahatika' kupata nafasi ya kwenda Ulaya kufanya kazi ni Sunday Bekunda (25), mwanafunzi wa mwaka wa pili katika Chuo Kikuu cha Makerere, Kampala.
Kwa bahati mbaya 'neema' ya kwenda Ulaya iligeuka balaa baada ya kutekwa na kulazimishwa kufanya ngono na wanawake mbalimbali huku akirekodiwa kwenye kamera za video.
"Ilikuwa ni Januari 2013, nilipokutana na mwanaume mmoja anayeitwa Charles kutoka katikati ya Jiji la Kampala, ambaye aliniahidi kunipeleka Kenya kufanya kazi katika kiwanda.
"Sikujua kuwa Charles alikuwa msafirisha watu. Alikuwa anaonekana kama mzazi wa makamo aliyefanya kazi kwa miaka mingi.
"Nilifungua moyo wangu na kumweleza changamoto nyingi ninazopitia na namna nilivyo hangaika kutafuta kazi ili nipate fedha za kulipia masomo ya ziada. Kwa kifupi ni kama nilikuwa namwambia Charles kuwa sikuwa natafuta kazi bali nilikuwa nataka kazi yoyote."
Safari ya Kenya
"Siku iliyofuata nilikuwa tayari kwa safari na nilimkuta Charles akiwa kwenye gari la binafsi aina ya Toyota Noah. Alikuwa pamoja na wasichana sita na wavulana wawili. Alituambia kuwa tutaingia Kenya kwa kupitia mpaka usio rasmi unaoitwa Chepskunya.
"Tukiwa njiani, Charles alikuwa anaongea sana na kutusisitizia kuwa 'tusimwangushe' tukifika huko. "Tulipofika Kenya walituchukua na kutuingiza kwenye nyumba moja nzuri ya makazi ya watu, hapo tulikutana na wenzetu 15, wavulana wawili kutoka Rwanda na Wakenya 13."
Kutekwa
"Charles alituacha hapo tukiwa chini ya mwanamke mmoja na wanaume wanne wenye miili iliyojengeka vyema. Watu hao walianza kutupiga makofi na kutulazimisha tuvue nguo. Ndipo nilipobaini kuwa kilichoonekana kama ni safari sasa imegeuka utekaji
"Baada ya kupigwa tuliambiwa tutoe mifukoni kila kitu tulichokuwa nacho na kuweka juu ya meza. Nilishtushwa nilipoona vyeti vya wanafunzi wa Uganda kutoka Vyuo Vikuu vya Kyambogo, KIU (Kampala International University), Nkumba na UCU (Uganda Christian University). Hata vyuo vya Kenya vilikuwapo.
"Mwanamke alitutishia kutuua kama tusingetii walichosema. Kudhihirisha alichokuwa anamaanisha, alituonyesha mkanda wa video wa mtu akiuawa na kupasuliwa tumbo.
"Halafu wakaweka video vyingine iliyotuonyesha biashara tutakayokuwa tunaifanya, ambayo ni kuigiza picha za ngono."
Ratiba ya kufanya ngono
"Walituongoza hadi ghorofa ya juu na kutuweka katika vyumba tofauti. Katika chumba nilichokuwepo aliingia mtu na kuniambia nitoe nguo kisha akanipa chupi tatu zinazobana.
"Hicho chumba kilikuwa na mwanga mkali na kamera za CCTV katika kila kona. Baadaye wakamleta Bridget, mmoja wa wasichana niliotoka nao Uganda, kisha wakaniambia kuwa nipo huru kufanya naye ngono. Walipoondoka na kufunga mlango, Bridget alianza kulia na kupiga kelele.
"Matukio mabaya yalianza rasmi siku iliyofuata wakati yule mwanamke alipoingia kwenye chumba changu akiwa ameshika mikanda mitatu ya ngono. Baadaye waliletwa wanawake na wanaume niliokuja nao nikaambiwa nifanye nao ngono wakati watu wengine wakirekodi kwa kutumia kamera kubwa.
"Nilipoishiwa nguvu, yule mwanamke alitoka nje na kurudi halafu alinichoma sindano yenye dawa ambayo ilinifanya nipate nguvu tena na kuendelea. Nikapewa ratiba ya kulala na wanawake asubuhi, wavulana jioni (mashoga) na wanawake watu wenye umri mkubwa usiku.
"Wanawake hao walikuwa wanawalipa wale jamaa ili tufanye nao ngono. Kuna wakati nilikuwa nalazimishwa kulala na wanawake saba kwa siku huku nikipata maumivu makali."
Mauaji
"Baada ya wiki tatu wote tuliitwa sebuleni na kupewa taarifa kuwa mmoja wetu, aliyeitwa Sam Muteesi kutoka Uganda, alikuwa amekataa kuwatii kwa hiyo alitakiwa auawe mbele yetu. Walimfunga kwenye kiti, japokuwa alikuwa akiomba sana msamaha walimfunika usoni kwa kutumia begi hadi alipokufa.
"Kwa kipindi chote cha Januari na Februari 2013, nilikuwa nikifanya ngono za kila aina kila siku huku nikitumia dawa za kulevya na pombe
"Mwanzoni mwa Machi, Charles alikuja kwenye chumba changu na kuniambia kuwa ninatakiwa kwenda kuoa Uingereza. Halafu akafungua kompyuta yake na kunionyesha picha ya mwanaume mzee mzungu.
"Akaniambia nipite mbele ya kompyuta hiyo nikiwa nimevaa chupi nilizopewa ili huyo mzungu anione (kupitia Skype) kama nifaa.
"Huyo mzungu alinipenda, hivyo Charles akawa amepata 'dili' ambayo ingenipeleka Uingereza, lakini kwa kuwa sikuwa Mkenya nilitakiwa nirudi Uganda kuchukua hati ya kusafiria.
Atoroka
"Wakati tukivuka mpaka kuingia
Uganda, nilifanikiwa kukimbia pale Mbale tulipokuwa tumesimama kunywa chai. Nilitoa taarifa yangu na kufunguliwa faili namba SD REF 65/19/03/2013. Kwa kuwa Charles alikuwa mtu mwenye nguvu (kifedha) hakufanywa chochote.
"Kutokana na mateso niliyopitia nilikuwa kama kichaa, nililazwa katika Hospitali ya Vichaa ya Butabika na nilipewa matibabu kati ya Agosti na Desemba 2013.
"Pia nilipimwa vipimo vingine na kugundulika kuwa nilikuwa na maambukizi yote makubwa ya magonjwa ya zinaa."Nimeamua kusimulia habari yangu kama sehemu ya kampeni ya kuwaonya vijana wa vyuo vikuu kuwa makini na watu wanaowaahidi kuwatafutia kazi nje ya nchi."
Imeandaliwa na Goodluck Eliona kwa Msaada wa Redio Netherlands Worldwide (RNW)
Share to:

Jumapili, 10 Agosti 2014

MAAJABU YA MUAROBAINI

Maajabu Tiba ya Muarobaini
Ndugu msomaji, Unaujua muarobaini...?
Wengi wetu watasema wanaujua lakini hawajui maana ya kuitwa muarobaini mti huo kwa kuwa mti huu ulipandwa nchini kwa amri ya kila nyumba kuwa na miti hii japo miwili huku wenye maeneo ya biashara wakihimizwa kuupanda mti huu kwa masharti kuwa asiyepanda basi atanyang’anywa leseni!
Si maneno ya mtu mwingine bali Kanali Yusuph Makamba ambaye aliwahi kuwa mkuu wa mkoa huu wa Dar Es Salaam enzi hizo za mwanajeshi huyu alipopata wazo la kuleta mbegu hii toka nchini India na kuupandikiza kijeshi-jeshi maana anatujua fika watanzania kwa ubishi usio na maana hata kwa maslahi yetu wenyewe.
Leo hii hasa vipindi hivi vya jua kali utakuta watu wote wapo chini ya muarobaini wakipata oksijeni nyiiingi tu toka kwenye mti huo jeuri bila kumbukumbu kuwa ulipandwa kwa viboko! Lakini, Angalau dozi ya malaria sasa inagusa mitaa ya shilingi elfu kumi na zaidi huku watanzania bado wanashindwa kutegua kitendawili cha mwanajeshi huyu mstaafu. Yeye amemaliza kazi:
Alikoutoa huo mti nchini India, unaitwa village Pharmacy na mlipomuuliza huu ni mti gani aliwajibu kuwa huu ni muarobaini na alijua mtalishika hili jina hadi mtakaposhindwa kumudu gharama za mahospitalini basi kila mtu atajua mwarobaini ni nini kwa kuwa utatibu maradhi yote yatakayotusumbua watanzania na kutunusuru na gharama hizi kubwa za madawa ya kemikali mahospitalini.
Nasikitika kuwa inawezekana siku tutakapolijua hili pengine mtaalamu huyu toka jeshi la Tanzania anaweza akawa kaburini na tukabaki na historia yetu ya kutangaza wema wa mtu baada ya kifo chake…
Muarobaini ukikamuliwa juisi yake umethibitishwa na vyuo vikuu vya tiba duniani kuwa una uwezo wa kukinga maambukizi ya HIV nap engine kutibu kabisa ugonjwa wa UKIMWI ambao husababishwa na virusi vya HIV.
Muarobaini una uwezo mkubwa wa kuzuia aleji na kutibu pia aleji za aina tofauti kama juisi yake itapakwa mwilini na hata kama utainywa pia.
Muarobaini huko Marekani na India umeonyesha uwezo mkubwa wa kuzuia nyani dume kutoa mbegu za uzazi kwa majike na kugundulika kuwa juisi ya muarobaini inamfaa mwanaume anayetaka kupanga uzazi bila kwenda hospitali kwa vipimo, ushauri na kufanyiwa upasuaji mdogo kukinga uzalishaji wa mimba (Vasectomy)
Muarobaini pia ni kiboko kwa wanawake wasio na mpango wa kushika mimba vilevile. Muarobaini kama utakamuliwa juisi yake na kupakwa kwenye via vya uzazi vya mwanamke , basi juisi hiyo itamsaidia mwanamke kutopata mimba zisizotarajiwa.
Muarobaini una uwezo mkubwa wa kupambana na kansa na hata kinga ya mwili pia. Tindikali ziitwazo Polysaccharides na limonoids zilizomo katika magamba, majani na mizizi huboresha kinga ya mwili haraka mno ili kupambana na maradhi kama kansa na mengineyo bila uharibifu wa mwili kama zilivyo dawa kemikali za mahospitalini.
Muarobaini hutibu kisukari kwa haraka sana. Majani matatu tu ya muarobaini ni dozi tosha kwa mgonjwa wa kisukari na akizidisha zaidi ya matatu basi anaweza kurudi hospitali na kuwaomba tena waganga waitafute sukari kwenye damu yake kwa tochi! Maana muarobaini utaikomba sukari yote kwenye damu hivyo usijiongezee dozi kijinga.
Muarobaini hushambulia wadudu wote wanaoshambulia ngozi ya binadamu kwa usahihi kabisa. Muarobaini hutibu mapunye, mba, ukurutu, upele na magonjwa kadhaa ya ngozi bila madhara yoyote.
Muarobaini hutibu magonjwa ya moyo. Huifanya damu kuwa nyepesi itembee kwa mwendo sahihi na kuyafanya mapigo ya moyo kuwa tulivu kwa wenye maradhi ya moyo.
Mafua. Ujerumani ambako ni nchi ya baridi kwa kipindi kirefu cha majira ya mwaka watu hufa kwa mafua tu! Tafiti walizofanya zinasema juisi ya muarobaini hukata mafua haraka zaidi ya dawa yoyote ya hospitalini huku ikikuhakikishia usalama bila madhara.
Muarobaini unaua fangasi. Inawezekana una fangasi miguuni, kwenye maungio ya siri kama mapajani, kwapani, sehemu za siri n.k. tumia juisi ya muarobaini ujipake sehemu zilizoathirika kupambana na fangasi hao bila madhara.
Muarobaini pia ni dawa ya kufukuza wadudu bila madhara ya kemikali. Jaribu kulala chini ya muarobaini lakini angalia pawe na majani yake hapo chini halafu utaona hakuna usumbufu wa mbu wala nzi maana mwarobaini hufukuza wadudu aina kadhaa akiwemo mbu!
Wakala wa kulinda mazingira Marekani imeupitisha muarobaini kama kinga bora ya kuhifadhia mazao dhidi ya wadudu waharibifu huku ikidaiwa kwamba muarobaini hauna sumu mara 200 zaidi ya madawa ya kemikali na mazao yanakuwa salama kwa matumizi ya binadamu,ndege na wanyama kwa ujumla.
Muarobaini pia hutibu malaria. Mchanganyiko maalum wa majani ya muarobaini uitwao kwa kitaalam “irodin A” ni sumu ya kuzuia na kutibu malaria. Majaribio mengi yamefanyika hata hapa nchini na muarobaini umeonekana una nguvu ya kupambana na malaria hata hapa nchini Tanzania japo si mti wenye asili yetu.
Nilipoingia katika tiba asili, wataalamu wengi waliniambia kama nataka mafanikio ya haraka basi nianze na kutibu wagonjwa kwa muarobaini. Naapa kwa watanzania wote kuwa nilifanikiwa sana maana hakuna aliyerudi akasema hakupona ugonjwa wowote hivyo nina imani siku mwarobaini ukitumika kama India basi utaitwa National Pharmacy….
Na nina wasiwasi kuwa kama wadau wa afya wakichelewa kuwajulisha wenye nchi taarifa hii muhimu tena kwa vituo basi watakapogundua hili, matabibu wengi watakosa ajira maana hakuna atakayeenda tena hospitali: akatafute nini?
Maana hata urafiki kati ya matabibu na wenye nchi utapungua kwa kuwa watagundua kuwa walifichwa habari hizi ili wawe mitaji ya wadau wa afya ambao ni sisi! Binafsi nimeanzisha kozi ya kutengeneza vidonge vya muarobaini inayogharimu shilingi elfu sitini tu kwa wenye familia zenye msimamo na tiba asili ili kesho niweze kujitetea kuwa nilijitahidi kwa uwezo wangu kusambaza taarifa hizi kwa vitendo.
Je, wewe mdau wa tiba mwenzangu umechukua hatua gani? Nipigie tukutane ofisini siku ya jumatatu, jumatano na Ijumaa pale machinga Complex Ilala Dar Es Salaam tuyaongee kwa vituo. Ada ya mazungumzo ni shilingi elfu tano tu!
Asanteni kwa kunisoma na tuuenzi Muarobaini….
Tabibu John Haule
Machinga Complex, Kawawa road.
Room no. 35F, 36F and 37F
Kariakoo Dar Es Salaam

Ijumaa, 8 Agosti 2014

NYANI AJIPIGA PICHA

Mtandao wa Wikipidia umekataa kufuta picha ambayo Nyani ilijipiga ikisema kuwa kwa sababu picha hiyo ilipigwa na Nyani ambaye ni mnyama wala sio binadamu, basi inakuwa mali ya umma.Hii ni baada ya mpiga picha, mmiliki wa kamera iliyotumika na Nyani huyo kujipiga picha, kusihi Wikipedia kufuta picha hiyo na kudai kuwa Wikipedia ilikuwa inaingilia haki zake za umiliki wa picha hiyo.
Mpiga picha, David Slater, alikuwa akijaribu kunasa picha za Nyani kwa masaa kadhaa, wakati ambapo Nyani mmoja alichukua mojawapo ya kamera za David na kujipiga mamia ya picha.
Picha hiyo aliyojipiga Nyani bila shaka ni ya kusisimua na imempeleka David kuwa maarufu ulimwengu mzima.
La kusikitisha ni kuwa hatimaye Slater sasa amejipata katika mvutano wa kisheria na Wikimedia kuhusiana na ni nani hasa mmiliki wa picha hiyo.
David, ambaye hutegemea upiga picha kama jinsi moja ya kujikimu kimaisha, yuko makini kuhakikisha picha hiyo imeondolewa kwa tovuti ya Wikipedia mara moja, huku Wikipedia ikidai kuwa iwapo kuna mmliki wa picha hiyo basi ni Nyani aliyejipiga picha hiyo.
Mvutano wa kisheria ilirejelewa kuangaziwa kufuatia uamuzi wa Wikipedia kuchapisha maombi yote iliyopata kuhusu kufuta au kuhariri habari au picha au video zozote ilizoweka kwenye tovuti zao.
Mojawapo ya maombi hayo ni David Slater kutaka picha aliyojipiga Nyani kuondolewa kwenye tovuti ya Wikipedia mara moja kwani ikiwa kwenye tovuti hiyo iko wazi kwa umma.

Jumatano, 6 Agosti 2014

MAHAKAMANI KWA UBAKAJI


Turn off for: Swahili
Na Deonidas Mukebezi, Dar es Salaam
MKAZI wa Mbezi Luis Omary Kupaza (32), amefikishwa katika Mahakama ya
Hakimu Mkazi Kinondoni akikabilikwa na kosa la kumbaka mtoto
(jinalimehifadhiwa) mwenye umri wa miaka (14),
Akisomewa kosa lake jana mbele ya Hakimu Izhaq Kuppa, wakili wa
Serikali Masin Mussa, alidai kuwa tukio hilo lilitokea Disemba 2013
huko eneo la Mbezi Msigwa.
Musa alidai kuwa Mshtakiwa alimbaka mtoto huyo kisha kumsababishia
maumivu makali sehemu za siri.
Mshtakiwa alikana kutenda kosa hilo na upelelezi wa shauri hilo bado
haujakamilika ambapo Hakimu Kuppa alidai kuwa kwa mujibu wa shtaka
hilo linadhaminika kisheria hivyo alimtaka mshtakiwa awe na wadhamini
wawili wenye barua ya utambulisho pamoja na nakala ya vitambulisho
vyao pia watakao saini ya maandishi ya Sh laki tano kila mmoja.
Hata hivyo kesi hiyo imeahirishwa katika Mahakama hiyo mara baada ya
mshtakiwa kushindwa kutimiza vigezo vilivyoainisha na Hakimu. Kesi
hiyo imeahirishwa hadi Agosti 19 mwaka huu kwa ajili ya kutajwa.

Katika hatua nyingine,Meneja wa kituo cha mafuta cha Gudal kilichopo
Ubungo Kibangu pamoja na mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
(UCC-UDSM), wamepandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi
Kinondoni wakikabiliwa na mashtaka mawili likiwemo la kuiba fedha
taslimu Sh. Milioni 51.6 mali ya Kituo hicho.
Washitakiwa hao ni Meneja Saadi Mohamed (21)na Edwin Mbuya (21) ambao
ni wakazi wa Ubungo Kibangu Jijini Dar es Salaam.
Wakisomewa mashtaka yao jana mbele ya Hakimu Kwey Rusema, Wakili wa
Serikali Credo Rugaju, alidai kuwa katika shtaka la kwanza,
linalowakabili washtakiwa hao ni kula njama ya kutenda kosa ambapo
tukio hilo lilitokea kati ya tarehe na muda usiyojulikana maeneo ya
Kinondoni Wilayani hapo.
Katika shtaka la pili Wakili Rugaju alidai kuwa Julai 28 mwaka huu
washtakiwa waliiba fedha taslimu Sh 51,689,500 mali ya kituo cha
mafuta cha Gudal kilichopo Ubungo Kibangu.
Washtakiwa walikana kutenda kosa hilo na upelelezi tayari umekamilika
hivyo upande wa Jamhuri uliomba Mahakama hiyo iwape washtakiwa dhamana
kwa kuwa ni haki yao kisheria.
Hata hivyo Hakimu Rusema alidai kuwa kila mshtakiwa anatakiwa awe na
wadhamini wawili kwa kila mmoja na kati yao awe na hati ya mali
isiyohamishika au kuweka saini ya maandishi ya Sh Milioni 15.
Washtakiwa walirudishwa mahabusu kwa kushindwa kutimiza masharti ya
dhamana na kesi hiyo itakuja tena Agosti 19 mwaka huu kwa ajili ya
kusikilizwa maelezo ya awali

Jumanne, 5 Agosti 2014

RASIMU YA KATIBA INAPOKA MADARAKA YA WATAWALA WASEMA MTANDAO WA WANAFUNZI

Mtandao wa wanafunzi Tanzania umesema kuwa chanzo cha mgogoro unaoendelea kati ya wajumbe wa bunge maalum la katiba ni kutokana na ukweli kwamba rasimu ya sasa ya katiba ya jamhuri ya muungano wa Tanzania ina muelekeo wa kuwapokonya madaraka watawala ambayo walipewa katika katiba ya zamani na kuyarudisha kwa wananchi.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es salaam,Katibu wa mtandao huo wa wanafunzi bwana ALPHONCE LUSAYO alisema kuwa katiba ya zamani ilikuwa ni zao la watawala ambapo tar 16 march 1977 chini ya Rais Julius Kambarage Nyerere katiba hiyo ilitungwa na watu ishirini tu ndani ya masaa manne chini ya uenyekiti wa aliekuwa katibu wa ASP Shekh Thabit Kombo.

Alisema Tofauti kubwa imeonekana katika rasimu ya katiba ya sasa ambayo ni zao la watawaliwa inayoshirikisha mawazo ya wananchi wengi na kuleta msuguano ndani ya Bunge maalum la katiba.

Hata hivyo Mtandao huo umesema kuwa kuna dhambi ambayo ni ya kihistoria na haitaweza kufutika katika mioyo ya watanzania na haitaweza kusuluhishwa kwa maridhiano endapo mchakato wa kupata katiba mpya uliogharimu mabilioni ya Watanzania utakwama.

Aidha mtandao uliwataka wajumbe kuachana na maslahi ya makundi yao na kuwaka malengo ya pamoja ya kupata katiba mpya ambayo itakuwa ni katiba ya wananchi na sio katiba ya kikundi flani cha siasa

Jumatatu, 4 Agosti 2014

MANSOOR AKAMATWA NA SIRAHA NA RISASI ZAIDI YA 500

Zanzibar.-Waziri wa zamani wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar Mansour Yusuph Himid amekamatwa na Jeshi la Polisi kwa tuhuma za kumiliki silaha kinyume na sheria imefahamika visiwani humo jana.
Mansour ambaye alivuliwa uanachama wa CCM na kupoteza nafasi ya mjumbe wa Baraza la Wawakilishi Jimbo la Kiembesamaki, alikamatwa nyumbani kwake huko Chukwani na kufanyiwa upekuzi mkali na askari wa kikosi cha upelelezi wakiongozwa na Naibu Mkurugenzi wa Makosa ya Jinai Zanzibar, Salum Msangi.
Akizungumza na waandishi wa habari katika makao makuu ya Jeshi hilo, Naibu Mkurugenzi wa Upelelezi na Makosa ya Jinai Zanzibar Salum Msangi alisema Jeshi la Polisi lilipokea taarifa za kiintelejensia kuwa waziri huyo wa zamani anamiliki silaha kinyume na sheria.

Ijumaa, 1 Agosti 2014

MTANDAO WA ULIPUAJI WA MABOMU ARUSHA WANASWA

Mtanzania
WATU 19 wamekamatwa na Jeshi la Polisi mkoani Arusha, wakidaiwa kuhusika na uingizaji, ulipuaji na usafirishaji wa mabomu pamoja na kumwagia watu tindikali.
Watuhumiwa hao wanadaiwa kununua mabomu hayo Jamhuri na Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Burundi.
Chanzo cha kuaminika kutoka ndani ya Jeshi la Polisi Mkoa wa Arusha, kililiambia MTANZANIA kuwa watuhumiwa hao akiwamo Sheikh wa Msikiti wa Bondeni jijini hapa na mfanyakazi wa Benki ya Stanbic, walitiwa mbaroni na Jeshi la Polisi baada ya kufanya uchunguzi uliowezesha kunasa mawasiliano ya simu pamoja na mitandao ya kijamii.
Chanzo hicho kilisema kuwa, watuhumiwa hao hutumia madereva wa bodaboda kwenda kununua mabomu hayo na kuyapitisha kwenye mpaka wa Burundi na Tanzania wa Manyovu mkoani Kigoma.
Chanzo hicho kilieleza kuwa mabomu hayo na tindikali husafirishwa na mabasi hadi mkoani Arusha ambapo hutumika kwenye vitendo vya kihalifu.
Watuhumiwa hao wote kwa pamoja wanapandishwa kizimbani leo katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Arusha kujibu tuhuma zinazowakabili.
Habari zaidi zilidai kuwa mtuhumiwa mwingine, Yahaya Hassan Hela maarufu kama Sensei, ambaye ni kinara wa matukio hayo anaendelea kusakwa.
Hivi karibuni jeshi hilo liliwakamata watuhumiwa wengine sita na kuwafikisha mahakamani kuhusiana na mlipuko wa bomu uliotokea Julai 7, mwaka huu kwenye Mgahawa wa Vama eneo la Viwanja vya Gymkhana jijini Arusha.
Katika operesheni hiyo mkazi wa Sombetini, Yussuf Hussein Ali na mkewe, Sumai Yussuf Ali, waliokutwa wakiwa na mabomu saba ya kurusha kwa mkono, risasi sita na unga wa baruti vikiwa nyumbani kwao, nao watafikishwa mahakamani leo kujibu tuhuma hizo.
Akizungumzia operesheni iliyofanikiwa kunasa watuhumiwa 19, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha, Liberatus Sabas, alisema ushahidi uliokusanywa umebaini kati yao watuhumiwa 21 wanahusika na matukio ya ulipuaji mabomu na umwagaji wa tindikali jijini Arusha.
“Matukio hayo ni yale yaliyotokea mwaka 2012 na hivi karibuni. Watuhumiwa hawa wanatazamiwa kufikishwa mahakamani kesho (leo), kuungana na wenzao waliokwishatangulia ili kujibu mashtaka,” alisema Kamanda Sabas.
Kamanda Sabas aliwataja watumiwa waliokamatwa na matukio waliyohusika nayo kama ifuatavyo:-
Bomu nyumbani kwa Katibu wa Bakwata
Kamanda Sabas aliwataja waliohusika na tukio la ulipuaji wa bomu nyumbani kwa Katibu wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania Mkoa wa Arusha, Sheikh Abdulkarim Jonjo Oktoba 25, mwaka 2012 ni Yussuph Ally Huta (30), Kassim Ramadhan (34).
Wengine ni dereva wa bodaboda, Mustapha Mohamed Kiago (49) pamoja na Sheikh wa Msikiti Mkuu wa Ijumaa, Abdulaziz Mohamed (49) ambaye pia alikuwa Imamu wa msikiti huo.
Kanisa la Olasiti
Aliwataja waliohusika na tukio la ulipuaji wa bomu kwenye Kanisa la Mtakatifu Joseph Mfanyakazi la Olasiti jijini Arusha Mei 5, mwaka 2013, kuwa ni Yusuph Huta (30), Ramadhan Waziri (28), Abdul Humud (30) na Wakala wa Mabasi ya Mohamed Trans (ambaye amefikishwa mahakamani kwa kuhusishwa na bomu la Mgahawa wa Vama).
Wengine ni Jafar Lema (38), ambaye alikuwa Imamu wa Msikiti wa Quba (ambaye amefikishwa mahakamani kwa kuhusishwa na bomu la Mgahawa wa Vama), Said Mohamed Temna (42), (ambaye amefikishwa mahakamani kwa kuhusishwa na bomu la Mgahawa wa Vama).
Wengine ni Kassim Ramadhan (34), Abashar Omar (24), ambao ni madereva bodaboda, Abdulrahman Hassan (41), pamoja na mfanyakazi wa Benki ya Stanbic Arusha.
Wengine ni Morris Muzi (44), mkazi wa Kalinzi mkoani Kigoma, Niganya Niganya (28), mkazi wa Businde Ujiji Kigoma, Baraka Bilango(40), mkazi wa Kalinzi Kigoma na Hassan Omar (40).
Mlipuko mkutano wa Chadema
Alisema Jeshi la Polisi limewanasa watuhumiwa kadhaa ambao walihusika katika tukio la ulipuaji wa bomu Juni 15, mwaka jana kwenye mkutano wa kampeni za udiwani za Chadema.
Watuhumiwa hao ni Yusuph Huta (30), Abdul Humud (30), pia wapo Said Temba (42), ambao wamefikishwa mahakamani kwa kuhusishwa na bomu la Mgahawa wa Vama na Jafar Lema (38).
Wengine ni Imamu wa Msikiti wa Quba, Sheikh Abuu Ismail, ambaye amefikishwa mahakamani kwa kuhusishwa na bomu la Mgahawa wa Vama.
Wengine ni Kasim Ramadhan (34), ambaye ni dereva wa bodaboda, Ramadhan Waziri (28).
Alitaja watuhumiwa wengine kuwa ni Abashar Hassan Omar (24), Abdulrahman Hassan (41), mfanyakazi wa Benki ya Stanbic Arusha, Morris John Muzi (28).
Wengine ni Niganya Niganya (28), Baraka Bilango (40) na Hassan Omar (40).
Kumwagiwa tindikali Sheikh Makambawa
Katika tukio la Julai 11, mwaka jana la kumwagiwa tindikali Sheikh Said Makambawa wa Msikiti wa Morombo, Kamanda Sabas aliwataja watuhumiwa wanaodaiwa kuhusika na tukio hilo kuwa ni Yusuph Ally (30), Ramadhan Waziri (28), Kassim Ramadhan (34) na Jafar Lema (38) aliyekuwa Imamu wa Msikiti wa Quba.
Kumwagiwa tindikali Sheikh Mustapha
Katika tukio hilo lililotokea Februari 28, mwaka huu, watuhumiwa katika tukio hilo ni Yusuph Ally (30), Kasssim Ramadhan (34), Jafar Lema (38) na aliyekuwa Imamu wa Msikiti wa Quba na Hassan Mfinanga (57).
Tukio la Arusha Night Park
Katika tukio hilo lililotokea Aprili 13, mwaka huu, watuhumiwa ni Jafar Lema (38), Imamu wa Msikiti wa Quba, Ibrahim Lenard au Sheikh Abuu Ismail (37) ambao wote walifikishwa mahakamani.
Bomu nyumbani kwa Sheikh Sudi
Kamanda Sabas aliwataja watuhumiwa waliorusha bomu kwa Sheikh Sudi, Julai 3, mwaka huu kuwa ni Yahaya Twalib (37), Idd Yusuph (32), Said Temba (42) ambaye amefikishwa mahakamani kwa kuhusishwa na bomu la Mgahawa wa Vama.
Wengine ni Anwar Nasher Hayel (29), Jafar Lema (38) ambaye amefikishwa mahakamani, Hassan Mfinanga (57), Yusuph Ramadhan (23) na Abashar Omar (24).
Tukio la mabomu nyumbani
Alisema katika tukio hilo la Julai 21, la familia kukamatwa na mabomu saba, watuhumiwa ni Yusuph Huta (30) na mkewe Sumaiya Yusuph Ally (19), Ramadhan Waziri (28), Hassan Ally Mfinanga (57) na Abashar Hasan Omar (24) ambaye ni dereva bodaboda.
Wengine ni Kimoro Mcahan (25), Hassan Omar (40), Morris Muzi (44), Niganya Niganya (28), Muha na mkazi wa Businde Ujiji mkoani Kigoma na Baraka Ntembo Bilango (40) Muha na mkazi wa Kalinzi Kigoma.
Kosa la kuhamasisha ugaidi kwa mtandao
Alisema jeshi hilo linawashikilia baadhi ya watuhumiwa kwa kuhusika na kosa la kuhamasisha vitendo vya kigaidi kupitia mitandao ya kijamii.
Watuhumiwa hao ni Ibrahim Lenard au Sheikh Abuu Ismail (37), Anwar Nasher Hayel (29) na Yasini Mohamed Shaban (20) mkazi wa Kaloleni.
Kamanda Sabas aliendelea kueleza kwamba, operesheni ya kuwatafuta watuhumiwa wengine wa matukio hayo inaendelea nchi nzima.
“Tunayo majina ya watuhumiwa kadhaa ambao wametoweka Arusha na kwenda kujificha maeneo mbalimbali ndani na nje ya nchi. Mtuhumiwa mmoja wapo anayetafutwa sana na polisi kuhusiana na matukio haya ni Yahaya Hassan Hella (Sensea) Mrangi ambaye ni mzaliwa wa Kijiji cha Chemchem wilayani Kondoa,” alisema Kamanda Sabas.
Alieleza kwamba, mtuhumiwa huyo ndiye kinara wa matukio ya milipuko ya mabomu na tindikali jijini Arusha kwa kushirikiana na watuhumiwa wengine waliokamatwa huku wengine wakiendelea kutafutwa.